Wamekula ya Mbuzi ...Wanaota Mapembe

Migogoro mingi katika bara la Afrika hutokea kwa sababu ya Madaraka, Viongozi wengi wanapotaka kuingia madarakani hutoa ahadi zenye kuvutia kwa wananchi wao lakini mara wanapoingia madarakani utamu wa madaraka huwazidi na kujikuta wakijaribu kadri wawezavyo kubadilisha Katiba ili waendelee kuongoza. Hali ambayo huzusha migogoro. Ama kweli "Wamekula ya Mbuzi sasa Wanaota Mapembe".

Monday, October 30, 2006

Kimya kingi

Nilikuwa katika safari ndefu ya kutembelea mashamba yangu ya huko Kapunga ambayo serikali ilitaka kutoa zawadi kwa mwekezaji, lakini kwa sasa nimerudi na niko fiti kwa ajili ya kuendela na kijiwe changu.

pia nawaomba radhi wasomaji wangu kwa kuwa nimekuwa kimya kwa muda huo wote bila kuwaletea mpya zozote katika kona yangu.

Monday, June 26, 2006

Bajeti ya Waziri Mkuu Hii Hapa!

Wapenzi wapitiaji wa kijiwe changu, nitakuwa nawapatia hotuba mbalimbali za mawaziri watakazokuwa wanazitoa hapa Bungeni mjini Dodoma kuhusiana na Bajeti za wizara zao, kwa jinsi nitakavyokuwa nazipata.

Kwa leo naanza na hotuba hii ya Waziri Mkuu Bw. Edward Lowassa.

Isome HAPA

Sunday, May 28, 2006

Ufukala umetukuta!

Nahisi hali inavyokwenda sio nzuri, kwa mtanzania wa kawaida kuweza kuhimili maisha ambayo yanazidi kuwa magumu zaidi kila kunapokucha.

Hebu fikiria pamoja na ugumu wa maisha uliopo sasa unaotokana na ukame na upungufu wa chakula ulioikumba nchi yetu na baadhi ya nchi jirani, limejitokeza tatizo lingine ambalo ni sawa na kupigilia msumari ndani ya kidonda!, tatizo hilo ni kupanda kwa bei ya mafuta.

Bei hiyo imekuwa ikipanda kila kunapokucha na kufikia kipindi ambacho mwananchi wa kawaida kushindwa hata kulipia nauli ya Daladala kwa sababu ya nauli kupanda mara kwa mara.

Kwa hali hii mtanzania hatakuwa na maisha bora hata siku moja kwani Njaa+ bei kubwa ya mafuta = Ufukara uliokithiri.

Thursday, April 13, 2006

Muda mimba inatungwa ndio wa kuzaliwa mtoto?

juzi nilikuwa nimekaa kwenye kijiwe cha kahawa kama Bw. Ramadhan Msangi anavypenda kukiita kijiwe cha "Ghahawa" huku nikiwa naendelea kupata kikombe kimoja baada ya kingine.

Baada ya muda mfupi walipita kinadada wawili ambao walikuwa wanabishana, mabishano ambayo yalikuwa yamekolea kiasi cha kushindwa hata kuniona mimi wakati napata kahawa katika kijwe chetu.

Mabishano na mada yao yalinivutia sana ndio maana nimeamua kuyapandisha katika kijiwe changu ili wageni wangu mnayetembelea kijiwe hiki mjaribu kuchangia.

Kinadada wale walikuwa wakibishana kuwa 'Eti muda ambao mimba inatungwa ndio muda huohuo mtoto atazaliwa?" kwani walidai kuwa hiyo ni kwa sababu watoto wengi wanazaliwa usiku ikiwa ni matokeo ya mimba nyingi kutungwa usiku.

Mimi sijui ila nawaomba wachangiaji wangu mjaribu kudadavua kuwa ni kweli juu ya mada hii?

Saturday, April 08, 2006

Azimio la Dodoma, ndio msimamo wetu!


Hivi karibuni kilifanyika kikao cha wanamtandao wa magazeti tando, katika kikao hicho kilichofanyika mjini Dodoma kilipitia na kuweka taratibu mbalimbali ambazo zinashauriwa kufuatwa na wanamtandao popote pale Duniani.

Soma hapa maazimio ya kikao hicho.

Katika picha hapo juu, kutoka kushoto ni Regnard Simoni, Hudson Kazonta, Martha Beatrice Mtangoo na Kipande ya jitu Mr. Mark Msaki, ambapo baada ya kikao wanamtandao walikuwa wakijadiliana baadhi ya mambo kwenye Kompyuta. (Picha kwa hisani ya Ibrahim Joseph)

Atapona mtu kweli!

Naanza kuandika kaujumbe haka kwenye kibaraza changu nikiwa na furaha tele moyoni, furaha ambayo miaka mingi ilifichika kutokana na maumivu ya dhuruma ambayo walala hoi tunafanyiwa na hawa wawekezaji hasa katika sekta ya madini.

Furaha hii inatokana na angalau kuahidiwa na mkuu wa nchi yetu Rais Kikwete alipokuwa akiwahutubia wananchi wa Botswana na kuwahakikishia kuwa mikataba yote iliyofungwa kwenye sekta ya Madini itapitiwa upya ili kuona ni jinsi gani inawafaidisha watanzania.

Hii kwangu ni furaha inayotokana na ahadi ya kupitiwa upya kwa mikataba hiyo kwani mingi imekuwa ikifungwa na kuwanufaisha wachache hasa wawekezaji pekee ambao imefikia kipindi wanatoa sababu za kiufundi kuhalarisha matakwa yao.

Kwa mfano kwa muda mrefu sasa baadhi ya migodi, baada ya kuchimbwa, mchanga hubebwa na kusafirishwa na kupelekwa nje ya nchi huku sisi tukiachiwa mashimo kwa madai kuwa hapa nchini hakuna teknolojia ya kusafisha mchanga huo.

Licha ya hiyo ni hivi majuzi tu yametokea mauaji yaliyolipotiwa na vyombo vya habari juu ya mchimbaji mdogo wa madini ya Tanzanite yanayodaiwa kufanywa na askari wa ulinzi wa kampuni moja ya uchimbaji madini huko Mererani, inayomilikiwa na wawekezaji.

Kwa kweli katika matukio kama haya watanzania wengi wamekuwa wakipoteza maisha yao kwa madai ya kulinda maslahi ya wawekezaji wasiokuwa na uchungu na nchi yetu na watanzania kwa ujumla.

Vilevile jambo la kushangaza ni kuwa mali zetu zilezile tulizoachiwa na babu zetu zimesababisha damu yetu imwagike kwa madai ya kulinda maslahi ya wawekezaji, kitu ambacho hakikubaliki kabisa kwani sidhani wenzetu mnayeishi huko ughaibuni kama mnapendelewa kama sisi tunavyowapendelewa wa nchi za magharibi.

Hivyo nina imani kuwa tamko la mkuu wa nchi litafanyiwa kazi kama alivyosema kuwa tayari wameanza kupitia mikataba hiyo ili kujua mustakabari wake na faida zake kwa nchi na watanzania kwa ujumla.

Pia ninachotaka kusisitiza kuwa wote watakaobainika kuwa walifunga mikataba hiyo kwa maslahi binafsi au kwa kujinufaisha wao wenyewe na familia zao, wachukuliwe hatua ikiwa ni pamoja na kufunguliwa kesi mahakamani ili warudishe mali za watanzania walizojinufaisha.

Kweli kwa hali hii viongozi wa serikali zilizopita wawajibike kwa kuingia mikataba inayowaumiza wananchi itakayogundulika baada ya kukamilika upitiwaji upya wa mikataba hiyo.

Friday, April 07, 2006

Kitimoto ni nini?

Nimepita moja wapo ya kibaraza nimekuta mabishano juu ya ukweli wa madhara yaliyopo ndani ya KITIMOTO kama wengi wanavyopenda kumwita japo mimi hujiuliza mara nyingi maana halisi ya neno hilo na kushindwa kuipata.

Katika mabishano hayo baadhi ya wachangiaji akiwemo Bw. Mkwinda alisema kuwa atahitaji siku moja kuwapata wataalamu wa afya ili watoe maelezo juu ya madhara ya nyama ya KITIMOTO kwani wengi wanahofia nyama yake kuwa ina madhara makubwa kwa afya ya binadamu.

Pamoja na hayo mimi sio daktari na sio nia yangu kuzungumzia madhara yaliyopo katika kitimoto, lakini ukweli ni kwamba nyama hiyo yaweza kuwa TAMU kuliko aina zingine za nyama hapa duniani.

Ukitaka kulijua hili siku moja tembelea kijiwe panapouzwa kitomoto halafu agizia nusu kilo pamoja na soda aina ya Coca cola, halafu taratibu anza kula kipande kimoja baada ya kingine ya nyama hiyo huku ukishushia na soda.

Sina shaka utafurahia kula nyama hiyo kwani imebarikiwa kwa kuwa na utamu wa pekee.

Pamoja na hayo nawaachia wasomaji wa kibaraza hiki swali kuwa "ni kwanini nyama hiyo ikaitwa KITIMOTO?"

Nimerudi!

Nimerudi!

Nimekuwa kimya kwa muda mrefu katika safu hii, hii ilitokana na kujiweka sawa zaidi katika kuwapatia wasomaji wangu na wapenzi wa kutembelea mtandao wa blogu vitu vipya na bora zaidi.

Kutokana na hali hiyo nimerudi upya katika safu hii ya kuwapatia habari mpya zenye mitazamo mbalimbali.

Karibuni sana.

Monday, January 02, 2006

Bila Utawala Bora ukeketaji kwa watoto wa kike hautakoma

WIZARA ya Maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto kwa kushirikiana na Mtandao wa Kutokomeza ukeketaji Tanzania, hivi karibuni iliendesha mkutano wa siku tatu katika ukumbi wa CCT mjini Dodoma uliokuwa na lengo la kujadili athari za mila hiyo hatari kwa wasichana na watoto wa kike.

Mila ambayo licha ya kupigwa vita na viongozi mbalimbali ikiwa ni pamoja vyombo vya habari na mashirika yasiyo ya kiserikali katika kila kona ya nchi ambayo jamii ya sehemu hizo inakumbatia mila hiyo, mila hiyo hatari inaonekana kuendelea kuwa sugu zaidi.

Mkutano huo ulihusisha wadau mbalimbali wanaopambana na mila hiyo yakiwemo mashirika mbalimbali yasiyo ya kiserikali yanayofanya shughuli zake za kupambana na mila hiyo katika mikoa ya Arusha, Kilimanjaro, Dodoma, Singida, Musoma, Iringa, Manyara,Tanga, Morogoro,Pwani, Dar es salaam na mikoa mingineyo ambako mila hiyo inafanyika zaidi ukilinganisha na mikoa mingine.

Baadhi ya mashirika yasiyo ya Kiserikali yanayopiga vita mila hiyo ni pamoja na AFNET Dodoma, WOWAP Dodoma, IAC matawi ya Dodoma, Kilimanjaro, Arusha, Tanga na Manyara, TAMWA, kituo cha sheria na haki za binadamu (LHRC), NAFGEM, AFNET Singida, TGNP, TAWLA, AYOHEP, IRA na mradi wa utafiti na utunzaji wa nyaraka wa chuo kikuu cha Dar es salaam (WRDP).

Ikumbukwe kuwa kwa mara ya kwanza Tanzania ilianza kushughulikia tatizo la ukeketaji mwaka 1994, baada ya mkutano wa kimataifa wa Cairo Misri, ambao ulipinga ukeketaji na kuhusisha na uvunjaji wa haki za binadamu, kwani suala la hilo lilionekana linaathiri zaidi maendeleo ya wasichana na wanawake na inapingana na haki za binadamu.

Pia katika mkutano wa wanawake uliofanyika Beijing China mwaka 1995 suala hili lilijitokeza na kuonekana kuwa ni tatizo ambalo linazidi kuwadidimiza wanawake kwa kunyimwa haki yao na kuwaathiri zaidi kisaikolojia.

Pamoja na kupigwa vita vitendo hivyo toka wakati huo, hali ya ukeketaji imekuwa bado ikiendelea katika jamii ya Watanzania hasa katika baadhi ya mikoa nchini, ambayo imeonekana kuikumbatia zaidi mila hiyo na kwa sasa kuanza kuifanya kwa siri kubwa.

Katika mkutano wa Afrika wa Mtandao wa Kutokomeza Ukeketaji uliofanyika Jinja Uganda March, 2000 uliazimia kila nchi mwanachama iwe na tawi la mtandao huo ili iwe rahisi katika utendaji kazi wa kila siku na kuleta mafanikio katika vita dhidi ya mila hiyo.

Hivyo Desemba, 2001 katika Hotel ya Njuweni Kibaha Mkoani Pwani tawi la mtandao wa kudhiti ukeketaji Tanzania lilizinduliwa likiwa na wajumbe 15, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa serikali katika kupiga vita mila hiyo nchini na utekelezaji wa maazimio ya mkutano wa Afrika wa Mtandao wa kutokomeza mila hiyo.

Baada ya kuzinduliwa kwa tawi hilo nchini ambapo mwenyekiti wake ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto Bi. Hilda Gondwe, lilianza kufanya kazi yake kwa kutoa elimu na kuweka mikakati mbalimbali ya kuhakikisha kuwa mikoa inayoendeleza mila hiyo inaacha kufanya hivyo.

Mpaka sasa inaonesha kuwa Idadi ya mangariba waliosalimisha zana zao za kazi na kuacha ukeketaji katika mikoa ya Manyara (98), Dodoma (83), Singida (96) na kutoka katika mkoa wa Ruvuma ni Mangariba 202.

Katika mkutano huo wa mtandao wa kudhibti ukeketaji nchini ambapo mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bw.Musa Nkhangaa, akitoa hotuba yake ya ufunguzi aligusia suala muhimu sana katika vita ya kupambana na mila hiyo hatari.

Mkuu huyo alisema kama utawala bora utaimarika toka ngazi ya vitongoji, vita ya mila hiyo itakuwa na mafanikio makubwa kwani vitendo hivyo vinapofanyika jamii na viongozi wa sehemu husika hujua lakini huvifumbia macho.

Alisema kama viongozi katika ngazi za vitongoji na vijiji watakuwa na utawala bora basi kutakuwa na uhakika wa kushinda vita dhidi ya mila hiyo ambayo ni ukatili mkubwa kwa wanawake na watoto wanapofanyiwa vitendo hivyo.

Hapa napenda kumuunga mkono Mkuu wa Mkoa kwa kufichua ukweli juu ya tatizo hilo ambalo serikali na wafadhiri wamekuwa wakitumia fedha nyingi sana katika kupambana na mila hiyo, na bado inaendelea kufanyika.

Sikubaliani kuwa mtoto katika mtaa fulani atakeketwa halafu Balozi wa mtaa huo asifahamu kuwa kuna mtoto katika mtaa wake kafanyiwa kitendo hicho hatari ambacho huweza kumsababishia maumivu na hata kumuambukiza magonjwa mbalimbali ikiwemo UKIMWI.

Kuna kila sababu ya kuhakikisha kuwa viongozi hawa wanakuwa na elimu ya kutosha juu ya madhara ya mila hiyo ili wawe mabalozi wazuri katika kupiga vita ukeketaji ambao kwa sasa unafanyika kwa siri kubwa.

Kama kutakuwa na utawala bora kutoka ngazi hizo na viongozi hao wa mitaa wakagundua umuhimu wa kupiga vita mila hiyo hatari, Serikali pamoja mashirika yanayopiga vita, yatakuwa na kazi rahisi itakayofanikisha kumaliza kabisa tatizo hilo.

Kuhusu jambo hili serikali inatakiwa kuweka utaratibu maalum ambao utawabana viongozi wote wa mitaa na vijiji watakaoshindwa kutoa taarifa serikalini, ambao itabainika kuwa katika mitaa yao kuna watoto au wasichana wamefanyiwa ukeketaji.

Kwa kuwabana hivi ndio itakuwa rahisi kwao kutoa taarifa kwani kwa sasa inaonekana kama vile vita ya kupambana na mila hiyo inahusu viongozi wa serikali wa ngazi ya juu na si kutoka ngazi ya chini na mashirika fulani tu, hali inayosababisha jamii kuwa na mwitikio mdogo katika vita hiyo.

Katika utafiti wa mwaka 1996 uliofanywa na DHS ulibainisha kuwa ukeketaji umekithiri sana katika mikoa ya Arusha na Manyara 81%, Dodoma 68%, KIlimanjaro 37%, Iringa 27%, Singida 25%, Tanga 25%, Morogoro 20% na Dar es salaam 5.4% hali iliyoonesha kuwa kiwango cha ukeketaji nchini kipo juu sana kulingana na takwimu kutoka katika maeneo ya mikoa hiyo.

Hivyo kwa sasa baada ya serikali kuunga mkono vita dhidi ya ukeketaji, vitendo hivyo vimegeuka na kuanza kufanywa kwa siri zaidi hali inayosababisha madhara makubwa kwa waathirika wanaofanyiwa vitendo hivyo.

Imekuwa ni vigumu kwa mangariba wanaofanya vitendo hivyo kuwapeleka watoto na wasichana hao hospitali inapotokea matatizo, baada ya kuwafanyia vitendo hivyo kwa kuhofia kubanwa na sheria.

Hivyo hali imekuwa mbaya zaidi kuliko ilivyokuwa hapo awali ambapo wasichana waliokeketwa waliweza kupelekwa hospitali na kupata matibabu kama itatokea matatizo baada ya kufanyiwa kitendo hicho.

Vilevile kwa sasa watoto wadogo ndio hasa wanaofanyiwa vitendo hivyo ambao hawawezi hata kujieleza au kuhisi ni nini wanafanyiwa, hivyo kuwanyima haki yao msingi ya kutoa maamuzi kuhusiana na maumbile yao.

Kwa mfano hivi karibuni vyombo vya habari viliripoti habari kutoka Mkoani Singida ambapo mtoto mchanga alikeketwa, hali ambayo inasikitisha na kutisha kwa mtoto mdogo tena mchanga kufanyiwa kitendo hicho.

Hapa naungana na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma kwa kuwatupia lawama viongozi wa ngazi ya vijiji na vitongoji kwa kutokuwajibika vilivyo kuzuia mila hiyo hatari ambayo inazidi kushika kasi katika baadhi ya mikoa hapa nchini.

Pia naiomba Serikali kuweka mikakati maalumu ambayo itahakikisha kuwa viongozi hawa wa ngazi za vijiji na vitongoji wanashiriki vilivyo katika kuhakikisha kuwa vitendo vya ukeketaji havitokei tena katika maeneo yao.

Kwa kufanya hivyo ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa jamii juu ya madhara ya mila hiyo Serikali itakuwa imepiga hatua nzuri katika vita dhidi ya mila hiyo ambayo humnyima mwanamke haki yake.

Napenda kusisitiza kuwa kuendelea kwa mila ya ukeketaji nchini, viongozi wa ngazi ya vijiji na vitongoji wanawajibika kwa kuvifumbia macho vitendo hivyo huku wakielewa fika kuwa ni uvunjaji wa sheria na kinyume cha haki za binadamu kuendeleza mila hiyo.