"Kupanga ni Kuchagua"

Kila mwanadamu ana mamlaka ya kubadilisha maisha yake kwa kutumia mazingira aliyo nayo! Mipango mibovu ya maisha yake husababisha maisha yake kuwa mabovu na Mipango bora ya maisha yake husababisha maisha yake kuwa Bora. Hivyo basi chagua maisha yako unataka yaweje?

Monday, October 30, 2006

Kimya kingi

Nilikuwa katika safari ndefu ya kutembelea mashamba yangu ya huko Kapunga ambayo serikali ilitaka kutoa zawadi kwa mwekezaji, lakini kwa sasa nimerudi na niko fiti kwa ajili ya kuendela na kijiwe changu.

pia nawaomba radhi wasomaji wangu kwa kuwa nimekuwa kimya kwa muda huo wote bila kuwaletea mpya zozote katika kona yangu.

Saturday, April 08, 2006

Azimio la Dodoma, ndio msimamo wetu!


Hivi karibuni kilifanyika kikao cha wanamtandao wa magazeti tando, katika kikao hicho kilichofanyika mjini Dodoma kilipitia na kuweka taratibu mbalimbali ambazo zinashauriwa kufuatwa na wanamtandao popote pale Duniani.

Soma hapa maazimio ya kikao hicho.

Katika picha hapo juu, kutoka kushoto ni Regnard Simoni, Hudson Kazonta, Martha Beatrice Mtangoo na Kipande ya jitu Mr. Mark Msaki, ambapo baada ya kikao wanamtandao walikuwa wakijadiliana baadhi ya mambo kwenye Kompyuta. (Picha kwa hisani ya Ibrahim Joseph)

Saturday, October 15, 2005

Mkapa anayo nafasi ya kuwapa HakiElimu kujirekebisha

HIVI karibuni Rais Benjamin Mkapa, alipiga marufuku Taasisi ya HakiElimu kujishughukisha na masuala ya elimu katika kipindi cha siku 30 zilizosalia za uongozi wake, huku akiisukumizia lawama lukuki kuwa ni wapotoshaji wa maendelea ya sekta ya elimu nchini.

Akihutubia mkutano wa hadhara katika kijiji cha Ikulu ndogo ya Chamwino, mjini hapa, ulioandaliwa na wanakijiji kwa ajili ya kumuaga, Rais Mkapa, alisema taasisi hiyo imekuwa ikipotosha ukweli halisi wa hali ya elimu nchini na kuwashushia hadhi watendaji wake wakiwemo walimu.

Alisema hataki katika uongozi wake kusikia taasisi hiyo ikijihusisha na jambo lolote linalohusiana na elimu katika shule za hapa nchini na kuachia dhamana na majaliwa ya asasi hiyo mikononi mwa Rais wa awamu ya nne.

Alisema Hakielimu wamekuwa wakipotosha elimu ya Tanzania kwa kutoa matangazo ambayo kwa njia moja au nyingine yalikuwa yanawajengea wananchi hali ya kudai haki bila wajibu.
"Nasema katika uongozi wangu sitaki kusikia HakiElimu wanakanyaga katika shule zetu, ni wapotoshaji na ni ujinga kuwaruhusu watu kama hao," alisisitiza Rais Mkapa.

Alisema hata vumilia hata siku moja kuona ujinga huo ukiendelea katika nchi yake ambayo amepewa mamlaka na wananchi kuiongoza na kwamba hatua hiyo itaendelea hadi pale taasisi hiyo itakapo elimika na kuacha upotoshaji huo, na kuifanya Serikali kuangalia upya msimamo wake.

Alisema hata wafadhili wanaoifadhili taasisi hiyo, wanatafuta uwezekano wa kuboresha elimu yao huko kwao na kufikia kiwango kizuri na kuhoji kwanini wadharau juhudi za kuinua elimu zinazofanywa na Serikali ya Tanzania.

Alitumia nafasi hiyo kumpongeza Waziri wa Elimu na Utamaduni, Bw. Joseph Mungai kwa uamuzi wake wa kuipiga marufuku taasisi hiyo na kusema kuwa ni hatua sahihi. Hatua hiyo ya Rais Mkapa, imekuja baada ya asasi hiyo kulalamikiwa na Serikali kuhusu matangazo yake inayoyatoa katika vyombo vya habari kulenga kuipinga Serikali katika juhudi zake za kuiboresha elimu nchini.

Rais Mkapa pamoja na kuzungumzia mambo mengi kuhusiana na asasi hiyo alimtaka Waziri wa Elimu na Utamaduni, Bw. Joseph Mungai, kutobabaika katika uamuzi wake kwani imeonesha ni kiongozi shupavu na anayefaa.

Pamoja na kusema hivyo aliacha majaliwa ya asasi hiyo kwa Rais ajaye kama ataona mabadiliko yoyote ya kiutendaji katika asasi hiyo na kufikiria uamuzi wa kuirudisha tena kufanya kazi kwa mujibu wa taratibu za nchi.

Ninavyojua mimi kiongozi wa nchi akibariki jambo ndio uamuzi wa mwisho au ni amri, amri hiyo ilianzia kwa Wizara ya Elimu na Utamaduni na baadaye baadhi ya wananchi walisikika wakilalamika hatua hiyo na kuitaka Serikali kuangalia uwezekano wa kuiruhusu asasi hiyo kuendelea na kazi zake kama kawaida kabla ya sasa Rais Mkapa kubariki uamuzi wa Bw. Mungai.

Kutokana na agizo hilo bila shaka sasa asasi hiyo ya HakiElimu haitafanyi kazi tena kwa mujibu wa amri iliyotolewa na Rais Mkapa, katika kukanyaga katika shule mbalimbali nchini, ingawa bado wanaweza kuendelea na kazi zao za kawaida.

Uamuzi wa Rais Mkapa, huenda kwa njia moja au nyingine, ukawa uamuzi sahihi wenye lengo la kutetea maslahi ya nchi ambayo yanahakikisha kuwa taratibu za ndani ya nchi hazivunjwi na AZISE zilizoanzishwa nchini kwa lengo la kukuza maendeleo ya sekta mbali mbali.

HakiElimu pamoja na kuandaa na kutoa machapisho ambayo yalikuwa yanaipinga Serikali katika juhudi zake za kuendeleza elimu hapa nchini, ilifanya baadhi ya mambo ambayo yalikuwa yanaeleza hali halisi ya mazingira ya elimu nchini.

Katika baadhi ya mambo ambayo HakiElimu ilikuwa inafanya vizuri ni pamoja na kuonesha jinsi watoto walemavu walivyokuwa wanakosa haki zao kwa kuchanganywa na watoto wasio walemavu katika masomo yao.

HakiElimu kwa upande mwingine walijitahidi kuonesha ni jinsi gani pesa za MMEM zilivyokuwa zikiliwa na wafanyakazi wa ngazi ya juu katika Halmashauri za Wilaya kwa kuwaelekeza walimu sehemu za kununua vifaa vya shule.

Pia asasi hiyo ilikuwa inawasaidi wananchi kuibua hisia za kujua haki yao katika uendeshaji wa shule zilizopo katika maeneo yao ikiwa ni pamoja kujua mambo muhimu kama mapato na matumizi ya shule na taarifa muhimu.

Kwa upande mwingine asasi hiyo ilijaribu kuweka wazi baadhi ya kero za wanafunzi katika masomo yao kwa mfano, Serikali kudai kuwa haiwabagui watoto wenye walemavu na wasio na ulemavu wakati shule zinazojengwa zina ngazi ndefu ambazo zinawawia vigumu wanafunzi walemavu kuingia madarasani.

Yote haya yalikuwa mema ya asasi hiyo na mengine mengi ambayo yalifanywa katika mlolongo huo na ambayo sio rahisi kuyataja yote ili mradi kufikisha ujumbe kwa Watanzania kuhusiana na kero mbalimbali katika sekta ya elimu.

Lakini basi sidiriki kubeza uamuzi uliotolewa na mkuu wa nchi, juu ya asasi hiyo na naamini kuwa, amefikiria kwa makini, amepitia vigezo mbalimbali na kuamua kutoa uamuzi kama huo.

Nadhani mantiki ya Rais Mkapa ni kwamba asasi hiyo imekuwa pinzani kwa kila jambo linalofanywa na Serikali katika harakati zake za kuboresha elimu, pasipo walau siku moja kutamka kuwa kuna jambo katika elimu ambalo limewafurahisha au limefikia kiwango kizuri na cha kupongezwa.

HakiElimu pia ilitoa machapisho mbalimbali ya utafiti ambayo yalikuwa yanaipinga Serikali katika ukuzaji wa sekta ya elimu, machapisho hayo yalikuwa yanasambazwa mashuleni na yalikuwa yanawavunja moyo walimu pia kuwashushia hadhi zao katika juhudi za ufundishaji.
Kama alivyozungumza Rais Mkapa, wakati akitoa agizo hilo, alisema baadhi ya matangazo yake yalilenga kuwajengea tabia Watanzania ya kudai haki tu bila kuwajibika.

Kwa mujibu wa Rais Mkapa, si rahisi kupata haki bila kuwajibika, bali kinachotakiwa ni wajibu kwanza halafu haki inafuata, na pengine Serikali imebaini kwamba ungefikia wakati ambao wananchi wangepinga kila jambo linalofanywa na Serikali kuhusu elimu.

Pamoja na mambo hayo, bado HakiElimu wanao muda wa kufikiria na kujirekebisha pale walipokuwa wanakosea kwani kwa mujibu wa Rais Mkapa, Serikali itafikiria upya uamuzi wake pindi asasi hiyo itakapojirekebisha.

Katika hali halisi, Serikali ya awamu ya nne ambayo imebakiza kama mwezi mmoja tu kuingia madarakani, inaweza kufikiria kuiruhusu asasi hiyo kuendelea na uhusiano na ushirikiano na shule za nchini, kama itajirekebisha katika mambo ambayo yamesababisha kuzua mgogoro na Serikali.

HakiElimu isikate tamaa, kwa sasa ikae chini na kuangalia ni mambo gani ambayo walikuwa wanakwenda kinyume na taratibu za Serikali, na baada ya kuyarekebisha waombe tena nafasi ili waweze kuendelea na kazi zao kama kawaida.

Tunaihitaji sana HakiElimu katika kuikosoa Serikali kwenye mambo ambayo inakwenda kinyume na Sera zake, lakini hatua hii ichukuliwe kama changamoto ya kudumisha na kukuza ushirikiano baina yake na Serikali, lengo likiwa ni kukuza kiwango cha elimu nchini.

Kukosolewa ni jambo la kawaida katika jamii, hivyo HakiElimu wachukulie agizo hilo la Serikali kama chachu ya kutumia nafasi hiyo kujadili na kurekebisha makosa yaliyopo ili kufufua umpya ushirikiano baina yake na Serikali.

Monday, September 19, 2005

Kwa Muswati Raha sana





HUWEZI amini katika hali ya kawaida kwa nchi zetu za kiafrika jinsi zilivyoathirika na gonjwa la ukimwi ambalo siku hadi siku linazidi kuwa sugu na kupoteza maisha ya waafrika wengi hali inayosababisha kuwepo kwa mayatima wengi wanaoachwa na wazazi wao.

Pamoja na hali hiyo Swaziland, nchi ambayo ni mojawapo kati ya nchi zilizoathiriwa sana na ugonjwa huo inaonekana baado sana wananchi wake hawajapata mwamuko wa kutosha katika vita ya kupambana na ugonjwa huo.

Hapa nakuletea baadhi ya picha zilizopigwa za wasichana vigoli ambao walikuwa wakipita mbele ya mfalme wa nchi hiyo MUSWATI kwa ajili ya kuchaguliwa ili waolewe na mfalme huyo.

Katika hali hii najua kwa wengi ni mtihani mgumu kwani kama unavyoona mwenyewe picha hizo kama ndio ungekuwa wewe ungevumilia kweli vifaa kama hivi vikipita mbele yako na kama ungeweza kuvumilia hebu nisaidie kuchagua kimwana mmoja ambaye unadhani alikuwa Bomba kuliko wote.

Saturday, September 10, 2005

Mzee wa Kiraracha hatuendi hivyo.

Ni muda sasa toka pazia la kampeni kufunguliwa na kuruhusu wagombea wa nafasi mbalimbali za uongozi katika vyama vya siasa nchini kunadi sera zao kwa wananchi kabla ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 30 mwaka huu.

Ni katika kipindi hiki ambapo tumeshuhudia wagombea wakijitokeza majukwaani wakijinadi kwa wananchi, kila mmoja akijitahidi kuainisha sababu zinazomfanya awaombe wananchi kumpa nafasi ya kumchagua ili awe kiongozi wao katika kipindi cha miaka mitano ijayo.

Zoezi hilo pia limekuwa likienda sanjari na kuvinadi vyama vyao kupitia sera za vyama husika huku wagombea hao wakijitahidi kuainisha kile kilichoko ndani ya ilani au sera za vyama vyao, ambazo kwa ujumla zimelenga katika kumkwamua Mtanzania bila kujali kuwa ni kwa namna gani

Kwa kifupi ni kuwa, kipindi hiki ni muhimu sana kwa walio na hata wale wasiokuwa wanasiasa kwa ujumla, kwasababu pande hizo zote zinategemeana katika kufanikisha mchakato huu kwa ujumla wake.

Ni sawa na kipindi cha kukaribia msimu wa kilimo ambacho wakulima hukitumia kusafisha mashamba yao tayari kwa kupanda mbegu mvua zikianza.Kipindi hiki kinatumika kwa wanasiasa kuweka wazi mikakati yao ya baadae kwa wapiga kura wao ili waweze kuwachagua.

Umuhimu wa kipindi hiki hauishii hapo tu kwani kwa upande wa wananchi hutarajia kujulishwa kwa kina wapi tulipokwama, kwanini tumekwama na kuainishiwa ni nani, kwanini na kwa namna gani atawaongoza kujikomboa kutoka katika lindi la umasikini.

Kwa bahati mbaya katika kampeni hizi kunajitokeza vitendo visivyo vya kistarabu kwa wapiga debe au viongozi wa vyama husika katika nafasi mbalimbali, kukitumia kipindi hiki kwa kuchafua majina ya wengine badala ya kuweka wazi sera zao.

Katika ufuatiliaji wangu wa kampeni hizo toka zilipozinduliwa rasmi na Tume ya Taifa ya uchaguzi (NEC), kuna baadhi ya wagombea na vyama vyao ambao hawajawahi kupanda jukwaani na kutangaza sera zao au za vyama vyao na badala yake kuona wamepata ulingo wa kuikashfu serikali na wagombea wa chama tawala.

Ni vyema ikafahamika kuwa Watanzania wa sasa sio wale tuliokuwa tunawafahamu katika miaka ya sabini na themanini. Watanzania waliokuwa wakiishi kwa utamaduni wa "ndio mzee", ambao walikuwa hawana uwezo wa kuhoji jambo ila kukubaliana nalo kwa vile limetolewa na kiongozi wa ngazi ya juu pasipo kujali baya au zuri.

Si lengo langu kuelezea kila jambo na kwa kila chama bali nataka kuangalia mwenendo mzima wa kampeni kupitia chama cha TLP maarufu kama "Jogoo", kinachoongozwa na "Mtaalamu wa mabomu au mzee wa Kiraracha", Augustine Mrema, ambazo zilianzia mkoani Mwanza.

Kwa mfuatiliaji mzuri wa kampeni atakubaliana nami kuwa, Mheshimiwa huyu toka alipozindua kampeni zake hajawahi kupanda jukwaani na kunadi sera kwa mantiki halisi ya sera zenye mrengo wa kumkwamua Mtanzania, kuwa anatarajia kufanya nini kwa wananchi endapo atachaguliwa kuiongoza nchi, kama ipo basi ilikuwa ni kibwagizo tu baada ya kumaliza kuiponda serikali na Chama cha Mapinduzi na viongozi wake.

Hili liko wazi na halina ubishi na kwa wananchi alimopita Mrema wataniunga mkoni kuwa kila anapopanda jukwaani husikika akikipaka matope Chama cha Mapinduzi na mgombea urais kwa tiketi ya chama hicho Jakaya Kikwete kuwa ni wabadhirifu wala rushwa, wasiojali wananchi wake, hawafai kupewa uongozi na mambo mengineyo ili mradi nafsi yake iridhike kuwa amekiponda chama hicho vya kutosha.

Pia amesikika kila mkutano anaohutubia akiwanyooshea vidole vingozi wa dini wakiwemo maaskofu kuwa wao ndio watakao changia kushindwa kwake eti tu kwa sababu baadhi yao walikwisha sema 'Kikwete ni Chaguo la Mungu'.

Wananchi wengi husikika wakicheka na kushangilia anapohutubia haya, si dhani kama wananchi wanakuwa wameridhika na maneno yake au wanashangilia tu kuwa Mheshimiwa Mrema ni mtaalamu wa kusema porojo na wanajua kuwa hana sera.

Mara kwa mara amesikika akisema kuwa Kikwete si Kijana ni mzee ila sura yake inasaidiwa na mkorogo tu, hili nalo hunifanya nicheke na hatimaye mbavu zangu kuuma, kwani sera ya Mrema ni ukijana au uzee? na uzee wa Kikwete yeye unamuathiri nini?.

Haya ni maswali ambayo hujiuliza kila mara na kukosa jibu la uhakika kwani kwa mwananchi wa kawaida anayetoka nyumbani kwake kwenda kwenye mkutano wa hadhara tena wa Rais mtarajiwa hatarajii mtu huyo kuanza kumzungumzia mpinzani wake eti kuwa ni mzee kwani yeye hajui hayo!.

Nafikiri msemo mmoja wa zamani umempitia kando mheshimiwa huyu kuwa "Usiuze ng'ombe wako kwa kumponda wa mwenzio" kama yeye kaamua kuingia kwenye biashara hii basi aiuze kwa kutaja sifa za bidhaa yake na si kuiponda bidhaa ya CCM ambayo tayari iko sokoni.


Kwa njia moja ama nyingine atakuwa (bila yeye kujijua) anakijenga Chama cha Mapinduzi na kukipa sifa kubwa kwa wananchi kwani kukiponda tu bila kueleza sera zake ni sawa na kutwanga maji kwenye kinu kwani wananchi hawatajua waende wapi na itawabidi wabaki walipo CCM kwani wewe huweki wazi sera zako watakuchaguaje? wakati huna sera unazozitangaza kwao?.

Mtu au mgombea wa aina hii hutoa nafasi kwa wananchi kumtilia mashaka kuwa hata wakimchagua ataongozaje nchi wakati hana sera na kama anazo haziweki wazi kwa wananchi ili waziweke kwenye mizani na kupima uzito ni zipi zinafaa kati ya za chama chake na vyama vingine.

Ikumbuke kuwa viongozi wa dini ni watu muhimu sana katika kuleta amani katika nchi yetu na kama kwa sasa hana uhusiano nao na anawalaani kila mkoa anaopita itakuwaje kama atachaguliwa kuliongoza dola, si viongozi hawa watakuwa hatarini.

Mimi naamini kuwa maaskofu na viongozi wa dini hao ni miongoni mwa raia wa Tanzania hivyo wanayo haki ya kusema katika jamii jambo ambalo wanafikiria katika vichwa vyao ndio maana walisema kuwa Kikwete ni chaguo la Mungu kama wazo binafsi na lisilo wahusisha watu wengine au dini zao.

Kwa wafuatiliaji wa taarifa mbalimbali za vyombo vya habari, sidhani kama kuna mtu anayeweza kukubaliana na ukweli kuwa viongozi hao walifanya makosa kama anavyotaka kutuaminisha mgombea huyu, kwasababu hakuna hata sehemu moja ambako viongozi hao walisema kuwa misimamo yao ni misimamo ya waumini wao.

Hivyo isiwe sababu kuwa kwa vile baadhi ya viongozi hao walisema kuwa Kikwete ni chaguo la mungu basi ndio kweli limekuwa chaguo la Mungu ila chaguo hilo litajulikana hapo Oktoba 30 baada ya uchaguzi mkuu kufanyika ndipo tutajua chaguo la Mungu ni lipi.

Kwa hali hii naweza kusema kuwa ni kufilisika kimawazo, Mtazamo, sera na malengo ya hapo baadae kwa kiongozi mkubwa kama Mrema kwani haifai kupoteza muda wa wapiga kura wanaojitokeza kuja kukusikiliza kwenye mikutano yako badala yake hawapati kitu walichofuata (sera) na kupata kashfa zinazoelekezwa CCM.

Nakumbuka siku moja nilipohudhuria mkutano mmoja wa kampeni wa Mrema katika eneo la Mvumi misheni hivi karibuni mkoani Dodoma alipoanza kuhutubia na wananchi kumsikiliza walichoshwa na kashfa hizo na mmoja wao alipayuka na kusema "tunataka sera! na sio majungu".

Kwa hali ya kawaida hapo awali katika miaka niliyoitaja huko nyuma sikutegemea mwananchi katika eneo kama hilo kuuliza kitu kama hicho ila imefika kipindi ambacho wananchi wanahitaji kiongozi mwenye mitazamo inayoridhisha na malengo mazuri katika kuhakikisha kuwa maisha yao yanaboreka.

Hiyo inathibitisha kuwa wananchi wa sasa sio wa "Ndio mzee" bali ni wananchi ambao wanataka kujua kuwa utakapoingia madarakani utashirikiana nao vipi na utawafanyia nini sio wao watakufanyia nini na hasa wanachojali ni sera zenye kuleta maendeleo.

Hapa napenda kushauri kuwa kama ndio mwenendo mzima wa kampeni za Chama Cha TLP zitakuwa namna hii bila kuwa na mabadiliko ya kuanza kutangaza sera yake ni heri fedha zinazogharamia kampeni zitumike kwa njia nyingine kwani kampeni bila kunadi sera ni sawa kuwaibia Watanzania.

Ikumbukwe kuwa fedha za kampeni ambazo vyama mbalimbali vinavyoshiriki katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu, sio fedha kutoka kwa wahisani bali ni fedha zilizopatikana kutokana na kodi za Watanzania hao hao ambao mnawadanganya na ambao wanauchungu na kodi zao kwasababu hawaoni kama zinawanufaisha.

Vipo vyama vingi ambavyo vinafanya kampeni za 'Kugombania' badala ya kugombea kuingia Ikulu kwa kutokuwaeleza wananchi malengo yao bila kujua kuwa muda ni mfupi sana kama utatumiwa visivyo na ni mrefu sana kama utapangiliwa kwa njia nzuri kwa hiyo staili hii ya kampeni haifai na itafanya mpaka muda unakwisha wananchi ambao ndio walengwa hawajajua kuwa sera ya TLP na mgombea wake Mrema iko vipi.

Naamini kuwa chama cha TLP na mwenyekiti wake Augustine Mrema mna sera ya kutosha tena mpya kama Digrii yako iliyokuja kwa Faksi hivi karibuni tu ikimaanisha kuwa hata vumbi haijapata, hivyo muda huu ndio wa kunadi sera hizo na usitegemee kusoma magazeti ili kupata ushahidi wa kuiponda CCM na viongozi wake.

Pia acha kuwalaumu na kuwalaani viongozi wa dini kwani hata wao wanaweza kukulaani, badala yake wafikishie wananchi ujumbe wa chama chako katika mikutano unayoihutubia ili wajue kuwa umelenga nini katika miaka mitano ijayo.

Mzee wa Kiraracha tunataka sera zilizokufanya upande jukwaani kutuhutubia au wewe unapenda kupanda jukwaani na kuwatukana viongozi wa serikali kwa kuwatolea maneno ya kebehi wenzio haoo wanakata mbuga, na jua kuwa usije kumbuka shuka wakati kumekucha!

Friday, July 15, 2005

Mpwapwa wapata Askofu Mpya


Kanisa la Anglican Tanzania Dayosisi ya Mpwapwa limemchagua askofu mwandamizi mpya atakaye chukuwa nafasi ya Askofu wa sasa atakapomaliza muda wake hapo mwaka 2007.

Kwa mujibu wa Tarifa iliyotolewa na Kanisa hilo na Kutiwa saini na Katibu mkuu wake Dr.Akili Mwita jana ilisema kuwa Askofu huyo atachukuwa atachukuwa rasmi kiti cha uaskofu hapo mwaka 2007 baada ya skofu wa sasa kustaafu.

Taarifa hiyo ilisema kuwa Mchungaji Canoni Jacob Erasto Chimeledya (48) alichaguliwa tarehe 12/7/2005 na sinodi maalumu ya uchaguzi katika Kanisa Kuu la watakatifu wote mjini Mpwapwa, uchaguzi ambao pia ulihudhuriwa na katibu mkuu wa Kanisa Anglican Tanzania.

Uchaguzi huo ambao ulihudhuriwa na wajumbe wapatao 230 ulisimamiwa na Askofu wa Dudley Mageni wa D ayosisi ya morogoro na Askofu huo atachukuwa nafasi ya Askofu wa sasa Dr. Simoni Chimwanga.

Taarifa hiyo ilisema kuwa Ibada ya kumweka wakfu kuwa Askofu itafanyika Jumapili ya Tarehe 9/10/2005 ambayo itaongozwa na Mhashamu Askofu Mkuu Donald Mtetemela wa Kanisa Anglican Tanzania.

Canon Chimeledya alizaliwa huko Zoisa katika wilaya ya Kongwa 1958 na kupata Elimu ya Shahada ya Theolojia katika chuo Cha Paulo Mtakatifu huko Limuru nchini Kenya na baadae kupata Shahada ya Uzamili wa Theolojia katika chuo cha Virginia huko Marekani mwaka 2003.

Taarifa hiyo ilisema kuwa Canon Chimeledya ameshawahi kufanya kazi mbalimbali, kuwa kasisi wa mitaa na kwa sasa ni Mkuu wa Chuo cha Theolojia cha Mt. Filipo cha Kongwa, pia ameoa na ana watoto wanne.

Thursday, June 30, 2005

WANA-BLOG WALITOA RAMBIRAMBI KUPITIA BLOG KWENYE MSIBA WA MNARC VIVIEN FOE



Hawa ni baadhi ya wanaBlog waliomkumbuka mchezaji maarufu wa Timu ya Taifa ya Cameroon na Mchezaji mahili wa Manchester City, Marc Vivien Foe, aliyefariki uwanjani katika mechi kati ya nchi ya Ufaransa na Cameroon mwaka 2003.

Ni kifo cha kishujaa katika hali ya kawaida kwani alikuwa akitetea nchi yake kuweza kuingia fainali katika mashindano hayo.

Kwa wakati huo Marc Vivien Foe alikuwa mchezaji wa timu ya Manchester City Kiungo wa kutegemewa katika timu hiyo Soma hapa habari kamili.

HUU UKOMAVU WA KIUONGOZI



Katika nchi zetu nyingi za Kiafrika ni vigumu sana na ninaweza kusema kuwa hiwezekani kwa mataifa mengine isipokuwa tu kwa Rais aliyeonekana kuwa amekomaa kimsimamo na anaye lilia haki ya wananchi wake Huyu si mwingine ni Raisi wa Afrika ya Kusini Thabo Mbeki.

Mheshimiwa huyu pasipo lawama wala papara amemfukuza kazi Makamu wake wa Rais ndugu Jacob Zuma kwa kuhusishwa na ulaji wa rushwa katika uongozi wake.kitendo hiki si kigumu tu kwa mfukuzaji bali hata kwa wananchi wenyewe kukubaliana nacho kwani tumesha sikia kuwa baadhi ya vyombo vya habari vikitangaza kuwa Wapambe wake ambao ni miongoni mwa wananchi wa nchi hiyo wakipinga kufukuzwa kwake.

Hiki ndicho kilichonifanya hata mimi kukumbuka ile kashifa ya sukari ambayo iliishia kwa mhusika kuambiwa kuwa ajiuzuru kwa manufaa ya umma, kwa kweli uamuzi kama huu kwa nchi yetu bado ni kitendawili kwani yanafanbyika hata yaliyomakubwa zaidi ya hili la mheshimiwa Zuma lakini wahusika huambiwa wajiuzuru kwa maslahi ya Taifa.

Hivi hii ni kwa maslahi ya Taifa au yake Binafsi?, kwani yeye akijiuzuru taifa litafaidika vipi? zaidi ya kumwacha yeye akitumia tu yale mavumba ambayo ameyapata kutokana na ukiukaji wa sheria alioufanya? kwa nini aifukuzwe na kupelekwa mahakamani kama huyu Mh. Zuma?

Kwa kweli inawezekana kwa kiongozi kufanya kosa na kufukuzwa kama alivyofanya mwenzetu wa huko Afrika ya Kusini na kupelekwa mahakani, bali kinachofanya jambo hili lishindikane ni kulindana kwa baadhi ya viongozi ambao wanakuwa madarakani na kushindwa kutumia dhamana yao waliopewa na wananchi.